Ni nani ambae ni Mrithi wa Mtakatifu Petro?



MNAMO 2002, Papa Yohana Paulo wa Pili alimwandikia barua askofu wa Limburg, huko Ujerumani, akifutilia mbali uamuzi uliofanywa na askofu huyo kuhusu suala la kutoa mimba. Papa alianza kutoa maagizo yake kwa kusema kwamba anawajibu wa kuhakikisha kuwa “makanisa yote yako katika hali njema na yana umoja kulingana na mapenzi ya Yesu Kristo.” Alidai kuwa ana mamlaka ya kufutilia mbali uamuzi uliofanywa na askofu huyo kwa sababu akiwa papa, yeye ndiye “mrithi wa Mtakatifu Petro.”
Kulingana na tafsiri fulani ya Kanisa Katoliki, “Kristo alimweka rasmi Mt. Petro kuwa mkuu wa mitume wote.” Kanisa Katoliki linaendelea kudai kwamba “Kristo alisema kwamba Petro anapaswa kuwa na watu watakaomrithi katika cheo hicho; na kwamba maaskofu Waroma ndio warithi wake.”—New Catholic Encyclopedia (2003), Buku la 11, ukurasa wa 495-496.
Hayo ni madai mazito. Je, wewe mwenyewe umewahi kuchunguza ukweli wa madai hayo? Ona majibu ya maswali haya matatu: (1) Je, Biblia inaunga mkono dai la kwamba Petro alikuwa ndiye papa wa kwanza? (2) Historia inaonyesha nini kuhusu chanzo cha mfuatano wa mapapa? (3) Je, mwenendo na mafundisho ya mapapa yanaunga mkono dai lao la kwamba wao ni warithi wa Petro?
Je, Petro Ndiye Aliyekuwa Papa wa Kwanza?
Ili kuthibitisha kwamba kanisa limejengwa juu ya Petro, kwa muda mrefu Wakatoliki wametegemeza madai yao katika maneno ya Yesu kwenye Mathayo 16:18: “Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu.” (Union Version) Hata maneno hayo yameandikwa kwa Kilatini chini ya dari la kanisa linaloitwa St. Peter’s Basilica huko Rome.
Agustino, Baba wa Kanisa aliyeheshimiwa sana, wakati fulani alisema kanisa limejengwa juu ya Petro. Hata hivyo, mwishoni mwa maisha yake alibadili maoni yake kuhusu maana ya maneno hayo ya Yesu. Kwenye kitabu kinachoitwa Retractations, Agustino alisema kwamba kanisa, yaani, kutaniko la Kikristo, limejengwa juu ya Yesu na si juu ya Petro.*
Ni kweli kwamba mtume Petro anatajwa sana katika vitabu vya Injili. Yesu aliwachagua mitume wake watatu—Yohana, Yakobo, na Petro—wawe pamoja naye kushuhudia matukio kadhaa ya pekee. (Marko 5:37, 38; 9:2; 14:33) Yesu alimkabidhi Petro “funguo za ufalme wa mbinguni,” ambazo alitumia kufungua njia ya kuelekea kwenye Ufalme—kwanza kwa Wayahudi na watu waliogeuzwa imani, kisha Wasamaria, na hatimaye Watu wa Mataifa. (Mathayo 16:19; Matendo 2:5, 41; 8:14-17;10:45) Kwa sababu Petro alikuwa mchangamfu na alipenda kuongea na watu, mara kwa mara alitumika akiwa msemaji wa mitume wote. (Matendo 1:15; 2:14) Hata hivyo, je, mambo hayo yalimfanya Petro kuwa kiongozi wa kutaniko la kwanza?
Ni kweli kwamba mtume Paulo aliandika kuwa Petro alikabidhiwa “utume kwa wale waliotahiriwa.” (Wagalatia 2:8) Hata hivyo, muktadha wa maneno hayo unaonyesha kwamba Paulo hakuwa akimaanisha kuwa Petro ndiye kiongozi wa kutaniko. Maneno ya Paulo yalihusu jukumu la Petro katika kazi ya kuwahubiria Wayahudi.
Ingawa Petro alipewa majukumu makubwa, hakuna mahali popote katika Biblia ambapo anadai kuwa yeye ndiye kiongozi wa kutaniko, na hivyo kufanya maamuzi kwa ajili ya mitume wale wengine wote. Katika barua zake alijiita “mtume” na “mwanamume mzee,” naye hakuongeza jambo lingine lolote.—1 Petro 1:1; 5:1.
Historia Inaonyesha Nini Kuhusu Chanzo cha Upapa?
Wazo la kuwa na mapapa lilianza jinsi gani na wakati gani? Wazo la kwamba ilikuwa sawa kwa mtu mmoja kuwa na madaraka juu ya waamini wenzake lilianza wakati mitume walipokuwa wangali hai. Mitume walikuwa na maoni gani kuhusu jambo hilo?
Mtume Petro mwenyewe aliwaambia wanaume waliokuwa wakiongoza katika makutaniko wasiwe ‘wakipiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu’; walipaswa kuwa wanyenyekevu kwa mmoja na mwenzake. (1 Petro 5:1-5) Mtume Paulo alionya kwamba katika kutaniko, watu wangesimama ambao ‘wangesema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.’ (Matendo 20:30) Mwishoni mwa karne ya kwanza W.K., mtume Yohana aliandika barua ambamo alimshutumu vikali mwanafunzi aliyeitwa Diotrefe. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba mwanamume huyo ‘alipenda kuwa na mahali pa kwanza’ kutanikoni. (3 Yohana 9) Shauri kama hilo kutoka kwa mitume lilikuwa kama kizuizi, likizuia kwa muda tamaa ya wale waliotaka kuwa na madaraka.—2 Wathesalonike 2:3-8.
Muda mfupi baada ya mtume wa mwisho kufa, watu mbalimbali walianza kupata mamlaka. Kitabu The Cambridge History of Christianity kinasema: “Huenda hakukuwa na askofu aliyekuwa na nguvu au mamlaka huko Roma mwanzoni mwa karne ya pili.” Kufikia karne ya tatu, askofu wa Roma alijifanya mwenyewe kuwa ndiye mamlaka kuu, kwenye makanisa fulani.* Ili kuongezea uzito lile dai la kwamba askofu wa Roma ana mamlaka kubwa, watu fulani wamekusanya orodha ya mapapa waliomrithi Petro.
Hata hivyo, orodha hiyo haiwezi kuthibitisha dai hilo. Kwa nini? Kwanza, baadhi ya majina kwenye orodha hiyo hayawezi kuthibitishwa. Zaidi ya hilo, msingi wa orodha hiyo una makosa. Jinsi gani? Hata ikiwa Petro alihubiri jijini Roma, kama baadhi ya vitabu vya kilimwengu vya karne ya pili na ya tatu vinavyodokeza, hakuna uthibitisho wa kwamba alikuwa kiongozi wa kutaniko huko.
Uthibitisho mmoja wa kwamba Petro hakuwa kiongozi wa kutaniko la Roma ni kwamba wakati mtume Paulo alipoandika barua yake kwa Waroma, aliandika orodha ndefu ya Wakristo waliokuwa huko. Hata hivyo, hakumtaja Petro hata kidogo. (Waroma 16:1-23) Ikiwa Petro alikuwa kiongozi wa kutaniko, je, tunaweza kuwazia Paulo akimsahau au kumpuuza?
Ona pia kwamba, karibu na wakati ambapo Petro aliongozwa na roho ya Mungu kuandika barua yake ya kwanza, Paulo alimwandikia Timotheo barua ya pili. Katika barua hiyo, Paulo hakusita kutaja Roma. Paulo aliandika barua sita akiwa Roma, na katika barua hizo zote hakumtaja Petro.
Miaka 30 hivi baada ya Paulo kuandika barua zake, mtume Yohana aliandika barua tatu na kitabu cha Ufunuo. Hakuna mahali popote katika maandishi hayo ambapo Yohana anataja kwamba kutaniko la Roma lilikuwa ndilo maarufu zaidi, wala kumtaja yeyote kuwa kiongozi wa kutaniko hilo ambaye alikuwa na mamlaka kubwa na aliyedai kuwa mrithi wa Petro. Hakuna uthibitisho wowote katika Biblia wala katika historia unaounga mkono dai la kwamba Petro alijiweka mwenyewe kuwa askofu wa kwanza wa kutaniko la Roma.
Je, Mwenendo na Mafundisho ya Mapapa Yanaunga Mkono Dai Lao?
Tungetarajia kwamba mtu anayedai kuwa “mrithi wa Mtakatifu Petro” na “Mwakilishi wa Kristo” afuate mwenendo na mafundisho ya Petro na Kristo. Kwa mfano, je, Petro alikubali kutendewa kwa njia ya pekee na waamini wenzake? Hapana. Hakukubali kutukuzwa wala kuitwa majina ya cheo. (Matendo 10:25, 26) Namna gani Yesu? Alisema kwamba alikuja kuwahudumia wengine na si kuhudumiwa. (Mathayo 20:28) Kinyume cha hilo, mapapa wana sifa gani? Je, wanakataa umaarufu, vyeo vya juu, na kuepuka kuonyesha waziwazi utajiri na mamlaka yao?
Petro na Kristo walikuwa safi kiadili na walichangia amani. Linganisha sifa zao na yale ambayo kitabu kimoja cha marejeo cha Wakatoliki, Lexikon für Theologie und Kirche (Kamusi ya Theolojia na Kanisa), kinavyosema kuhusu Papa Leo wa Kumi: “Alijiingiza katika siasa na mara nyingi aliwapendelea watu wake wa ukoo katika shughuli za biashara na kupenda sana anasa. Kwa kufanya hivyo, Leo wa Kumi alipuuza mambo ya kiroho yaliyokuwa muhimu.” Karl Amon, kasisi Mkatoliki ambaye pia ni profesa wa historia ya kanisa, anasema kwamba habari zilizothibitishwa kuhusu Papa Aleksanda wa Sita zinaonyesha “uovu mwingi, matumizi mabaya ya mamlaka, kununua au kuuza vyeo katika kanisa, na upotovu wa maadili.”
Namna gani mafundisho ya mapapa? Je, yanapatana na mafundisho ya Petro na Kristo? Petro hakuamini kwamba watu wote wema wanaenda mbinguni. Akimrejelea Mfalme mwema Daudi, Petro alisema hivi waziwazi: “Daudi hakupanda mbinguni.” (Matendo 2:34) Wala Petro hakufundisha kwamba watoto wachanga wanapaswa kubatizwa. Badala yake alifundisha kwamba ubatizo ni hatua ambayo mwamini anachukua kwa kuongozwa na dhamiri yake.—1 Petro 3:21.
Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kwamba hakuna yeyote kati yao anayepaswa kuwa mkuu kuliko wengine. Yesu alisema: “Ikiwa mtu yeyote anataka kuwa wa kwanza, lazima awe wa mwisho kati ya wote na mhudumu wa wote.” (Marko 9:35) Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu aliwapa wafuasi wake agizo hili lililo wazi: “Msiitwe Rabi, kwa maana mwalimu wenu ni mmoja, lakini ninyi nyote ni ndugu. Zaidi ya hayo, msimwite mtu yeyote baba yenu duniani, kwa maana Baba yenu ni mmoja, Yule wa mbinguni. Wala msiitwe ‘viongozi,’ kwa maana Kiongozi wenu ni mmoja, Kristo.” (Mathayo 23:1, 8-10) Je, unafikiri mapapa wamefuata mafundisho ya Petro na Kristo?
Wengine wanasema kwamba mtu anaweza kuendelea kuwa papa hata ikiwa haishi kulingana na kanuni za Kikristo. Je, unafikiri hoja hiyo inapatana na akili? Yesu alisema: “Kila mti mzuri huzaa matunda mazuri, lakini kila mti uliooza huzaa matunda yasiyofaa; mti mzuri hauwezi kuzaa matunda yasiyofaa, wala mti uliooza hauwezi kuzaa matunda mazuri.” Ukitegemea uthibitisho ambao umetolewa, je, unafikiri kwamba Petro au Kristo wangependa kuhusianishwa na matunda ambayo mapapa wametokeza?—Mathayo 7:17, 18, 21-23.
[Maelezo ya Chini]
Mazungumzo ya Yesu na Petro yalihusu kumtambua Kristo na jukumu lake, na si kuhusu jukumu ambalo Petro angetimiza. (Mathayo 16:13-17) Baadaye, Petro mwenyewe alisema kwamba Yesu ndiye mwamba ambao juu yake kutaniko lingejengwa. (1 Petro 2:4-8) Mtume Paulo alithibitisha kuwa Yesu, wala si Petro, ndiye “jiwe la msingi la pembeni” la kutaniko la Kikristo.—Waefeso 2:20.
Yesu na mitume walionya kwamba kutaniko la Kikristo lingevamiwa na watu ambao wangefundisha mafundisho ya uasi. (Mathayo 13:24-30, 36-43; 2 Timotheo 4:3;2 Petro 2:1; 1 Yohana 2:18) Maneno hayo yalitimia wakati kanisa, au kutaniko, la karne ya pili lilipoanza kukubali mapokeo ya kipagani na kuchanganya mafundisho ya Biblia na falsafa za Wagiriki.
[Picha katika ukurasa wa 25]
Je, uthibitisho unaonyesha kwamba mapapa wameiga mfano wa Petro?


Comments

Popular posts from this blog

DOWNLOAD NA USIKILIZE NYIMBO ZA KWARESIMA